Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam ambae ni pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Amani ya Mkoa huo Walid Alhad Mussa Kawambwa amewataka viongozi wa Dini tofauti nchini kutumia nafasi zao kuhamasisha amani kwa waumini wanao waongoza hususani katika kipindi hiki ambacho Taifa linatarajia kuingia kwenye Uchaguzi Mkuu ifikapo mwezi Oktoba 2025.
Sheikh Kawambwa ameyasema hayo leo Aprili 23,2025 jijini Dar es Salaam katika Kongamano la Amani lililoshirikisha viongozi wa madhehebu wa dini tofauti kuelekea Uchaguzi Mkuu 2025 lililolenga kujadili mchango wao katika kudumisha utulivu na amani wakati wa uchaguzi.

Amesema nafasi ya kiongozi wa Dini katika kujenga au kubomoa amani ya Taifa , ni moja kati ya mada yenye umuhimu wa kipekee ambayo inawakutanisha Viongozi wa dini tofauti kukaa meza moja huku wakijenga tafakuri ya kutekeleza ajenda ya kuwaelimisha waumini wao juu ya suala zima la kulinda amani ya Taifa kwa nyakati tofuati.
"Imeandikwa katika vitabu vitukufu vya Mwenyezi Mungu ikiwemo Qur an, Biblia, Injili na Taulati kuwa suala la kudumisha amani kwenye Taifa lolote lile ni jambo la wajibu unaopaswa kutekelezwa kuanzia kwa viongozi wa dini hadi kwa waumini wao". Amesema 

Kwa upande wake, Askofu Philipo Mafuja wa Kanisa la AICT, Dayosisi ya Pwani, amewahimiza viongozi hao kuwa waangalifu na kauli zao hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, na kuepuka kuingilia majukumu ya vyombo vya usalama.
“Tunahitaji kuwa waangalifu na maneno yetu tunapowahutubia waumini. Tumepewa dhamana kubwa, hivyo ni wajibu wetu kutumia nafasi hiyo kueneza ujumbe wa amani na mshikamano,” amesema Askofu Mafuja.
Amesisitiza pia kwamba viongozi wa dini wanapaswa kuepuka kujihusisha moja kwa moja na siasa au kushiriki matukio ya kisiasa yanayoweza kuathiri taswira ya taasisi za kidini. “Ni muhimu kutambua kuwa misingi ya siasa haiwezi kuhamishiwa moja kwa moja kwenye dini,” ameongeza.
Katika kongamano hilo, pia ilijadiliwa nafasi ya wanawake katika siasa. Mwanaharakati wa haki za wanawake, Shamim Khan, ameeleza kuwa bado kuna vikwazo vinavyowazuia wanawake kushiriki kikamilifu kwenye siasa, kama vile lugha ya matusi na udhalilishaji wa kijinsia.

“Kwa hali ilivyo sasa, bado kuna umuhimu wa kuendeleza mfumo wa viti maalum kwa wanawake. Si wakati muafaka kuuvunja mfumo huo, kwani bado hatujafikia usawa wa kweli katika nafasi za uongozi,” amesema Shamim.
Aidha, amewahamasisha wanawake kujiamini na kushiriki kwa wingi katika michakato ya uchaguzi ili kuongeza uwakilishi wao katika vyombo vya maamuzi.