Breaking

Sunday, 6 April 2025

UCHAGUZI 2025: BALOZI NCHIMBI ATOA WITO

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi amesema kuwa msingi wa sera za CCM utabakia kuwa ni maendeleo ya watu pamoja na amani na utulivu wa nchi.

Balozi Nchimbi aliyasema hayo leo Jumapili, tarehe 6 Aprili 2025, alipokuwa akizungumza na mamia ya wananchi wa mji wa Songea katika maeneo ya Liziboni, Uwanja wa Majimaji na Mshangano, ambapo wananchi walikusanyika kwa hamasa kubwa kumsikiliza licha ya kuwa kwenye ziara nyingine za kikazi.

Katika eneo la Liziboni, Balozi Nchimbi alilazimika kusimamisha msafara wake ili kuzungumza na wananchi waliomsimamisha njiani akitokea Nyasa. Alitumia fursa hiyo kuwashukuru wananchi wa Songea kwa mchango wao mkubwa uliomuwezesha kufahamika kitaifa na kimataifa.

Katika Uwanja wa Majimaji, alihutubia umati mkubwa wa wananchi waliokuwa wakimsubiri wakati alipofika kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo la ghorofa lenye fremu 50 za CCM Mkoa wa Ruvuma. Katika hotuba yake, aliwaomba wananchi wa Songea, mkoa mzima na nchi nzima kwa ujumla kujiandaa kushiriki kwa wingi Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, 2025.

Akiwa Mshangano, ambako alizindua rasmi fremu 50 za tawi la CCM la eneo hilo, Balozi Nchimbi alisisitiza tena umuhimu wa ushiriki mkubwa wa wananchi katika uchaguzi mkuu, akieleza kuwa ni kwa njia hiyo ndipo maendeleo na ustawi wa taifa yanaweza kufikiwa kwa kasi na kwa manufaa ya wote.

Kwa ujumla, ziara ya Katibu Mkuu huyo ilionesha mapokezi makubwa ya wananchi na kiu ya kusikia mwelekeo wa chama chao kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages