Breaking

Friday, 11 April 2025

TEA KUTUMIA MILIONI 300 KUKARABATI JENGO LA BODI YA MAKTABA PEMBA

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) inaendelea na juhudi za kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji nchini kote. Katika jitihada hizo, TEA imetenga kiasi cha Shilingi Milioni 300 kwa ajili ya ukarabati wa jengo la Bodi ya Maktaba lililopo kisiwani Pemba. Ukarabati huu unalenga kuimarisha miundombinu ya taasisi hiyo muhimu inayotoa huduma kwa wanafunzi na wananchi kwa ujumla.

Akizungumza katika ziara ya ukaguzi kisiwani Pemba, Kaimu Mkurugenzi wa Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi kutoka TEA, Bw. Masozi Nyirenda, alieleza kuwa fedha hizo tayari zimetolewa. Alibainisha kuwa ukarabati utaanza mara tu baada ya mkandarasi kusaini mkataba rasmi na kuwasilisha mpango kazi utakaoonesha hatua kwa hatua namna kazi hiyo itakavyotekelezwa hadi kukamilika kwa wakati.

Mradi huu wa ukarabati unatekelezwa kama sehemu ya majukumu ya TEA kama taasisi ya Muungano, ambayo kimsingi inahusika na utafutaji wa rasilimali kutoka kwa wadau mbalimbali ili kusaidia jitihada za Serikali katika kuboresha miundombinu ya elimu. Kupitia miradi kama hii, TEA inalenga kuhakikisha kuwa kila mwanafunzi anapata mazingira bora ya kujifunzia bila kujali eneo analotoka.

Kwa mujibu wa Mratibu wa Bodi ya Maktaba Pemba, Bw. Ahmed Hamis, jengo linalotarajiwa kukarabatiwa ni miongoni mwa majengo ya kihistoria yaliyojengwa kipindi cha ukoloni. Hata hivyo, tangu lijengwe, jengo hilo halijawahi kukarabatiwa, jambo lililosababisha uchakavu mkubwa wa jengo zima na miundombinu ya ndani, na hivyo kuathiri utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bw. Hamis ameongeza kuwa kukamilika kwa ukarabati huo kutakuwa ni faraja kwa wakazi wa Wilaya jirani ambao hutegemea huduma za maktaba hiyo kwa ajili ya kusoma vitabu, hasa watoto wanaohitaji nyenzo za kielimu kama vile hadithi na historia za watu mashuhuri. Ukarabati huu unatarajiwa kuleta mwamko mpya wa elimu na kujifunza miongoni mwa wakazi wa Pemba.
Mratibu wa Bodi ya Maktaba Pemba Bw. Ahmed Hamis ( mwenye tisheti) akielekeza kitu kwa Kaimu Mkurugenzi Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi kutoka TEA Bw. Masozi Nyirenda, wakati wa ziara ya kukagua hali ya uchakavu wa jengo litakalofanyiwa ukarabati.
Muonekano wa hali ya uchakavu katika jengo la Bodi ya Maktaba - Pemba ambalo litafanyiwa ukarabati kupitia TEA

Mratibu wa Bodi ya Maktaba Pemba Bw. Ahmed Hamis ( mwenye tisheti) akielekeza kitu kwa Kaimu Mkurugenzi Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi kutoka TEA Bw. Masozi Nyirenda, wakati wa ziara ya kukagua hali ya uchakavu wa jengo litakalofanyiwa ukarabati.



Muonekano wa hali ya uchakavu katika jengo la Bodi ya Maktaba - Pemba ambalo litafanyiwa ukarabati kupitia TEA




Ukaguzi wa jengo la Bodi ya Maktaba Pemba ukiendelea kuona hali halisi ya uchakavu kabla ya ukarabati kuanza.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages