
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe Judith Kapinga amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme kwenye maeneo ya migodi midogo yakiwemo maeneo yanayozalisha chumvi wilayani Bagamoyo.
Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Aprili 08, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la la Mbunge wa Bagamoyo, Mhe. Muharami Shabani Mkenge aliyeuliza ni lini Serikali itapeleka umeme katika eneo la Kitame Kata ya Makurunge wilayani Bagamoyo ili kuwasaidia wazalishaji wa chumvi.
"Hadi kufikia mwezi Machi 2025, jumla ya maeneo 14 ya migodi midogo imepelekewa umeme ambapo kati ya hayo, maeneo 3 ni ya wachimbaji wa chumvi wanaopatikana katika eneo la Kitame Kata ya Makurunge ambapo jumla ya wachimbaji 34 wanaopatikana katika maeneo hayo wamefikiwa na huduma ya umeme". Amesema Mhe. Kapinga
Ameeleza kuwa, kazi ya kupeleka umeme kwa wachimbaji wa chumvi waliosalia itaendelea kulingana na upatikanaji wa fedha.
Ameongeza kuwa, upo mradi mwingine ambao unapeleka umeme kwenye pampu za maji takribani 411 na kwenye maeneo ya kilimo na maeneo ya migodi 605.
Akijibu swali Mbunge wa Kibiti, Mhe. Twaha Mpembenwe aliyeuliza kuhusu mkakati wa Serikali kupeleka umeme kwenye Kitongoji cha Kitame ili wananchi waweze kunufaika na uwepo wa nishati hiyo, Mhe. Kapinga amesema katika eneo hilo Serikali inatekeleza miradi ya umeme ya Vitongoji.
Katika hatua nyingine Mhe. Mpembenwe kwa niaba ya wananchi wa Kibiti amemuomba Mhe. Judith Kapinga kufikisha pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa miradi ya umeme ya zaidi ya shilingi Bilioni 3.8 katika Jimbo la Kibiti.
Mhe. Kapinga kwa upande wake, amesema Serikali inapokea pongezi za wananchi hao wa Kibiti kwa Mhe. Rais kutokana na kazi kubwa anayoifanya katika sekta ya nishati ambayo inasimamiwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Doto Biteko.
Akijibu swali la Mbunge wa Urambo, Mhe. Margreth Sitta aliyeuliza ni lini Serikali itakizindua kituo cha kupokea na kupoza umeme cha Uhuru kilichopo Urambo Tabora baada ya kukamilika, Mhe. Kapinga amesema kituo cha kupokea na kupoza umeme cha Uhuru kimekamilika Machi 26, 2025 na wananchi wa Urambo, Kaliua na maeneo jirani wananufaika kupitia kituo hicho cha umeme.
Akijibu swali la Mbunge wa Kilombero, Mhe. Abubakar Asenga aliyetaka kufahamu ni lini mkakati wa kuvipelekea umeme Vitongoji 15 kwa kila Mbunge utaanza jimbo la Kilombero, Mhe. Kapinga amesema tayari Serikali imeshampata Mkandarasi wa kupeleka umeme katika Jimbo hilo na ameshaanza kazi katika baadhi ya maeneo na Serikali itaendelea kumsimamia ili aongeze kasi ya utekelezaji wa mradi huo.