HALI ya upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam imeimarika kufuatia kukamilika kwa marekebisho ya mtambo mmoja katika mitambo ya kuzalisha maji katika eneo la Ruvu Juu huku kiwango cha maji katika mto Ruvu kikiongezeka.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 7, 2025 Jijini Dar es Salaam, Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), Mhandisi Mkama Bwire amesema wananchi hawapaswi kuwa na hofu kutokana na hali ya maji kuendelea kuimarika ikilinganishwa na wiki chache nyuma ambapo pia baadhi ya maeneo ambayo yalikosa maji yameanza kupata ikiwemo maeneo ya Tabata, Kinyerezi, Mbezi Makabe na maeneo ya Mshikamano.
Amesema kuwa hali ya maji katika Mto Ruvu iko katika kiwango kizuri cha uzalishaji, na changamoto iliyotokea hivi karibuni katika Mtambo wa Uzalishaji Maji wa Ruvu Juu tayari imeshughulikiwa kikamilifu, hivyo shughuli za uzalishaji na usambazaji wa maji zinaendelea kama kawaida.
Aameongeza kuwa DAWASA inaendelea na jitihada za kusambaza maji kwa wananchi wote, hasa katika maeneo ambayo yalikuwa na changamoto za upatikanaji wa huduma kama Kinyerezi, Makabe, Mshikamano, na Machimbo. Amesema huduma katika maeneo hayo imeanza kuimarika kwa kasi.
Aidha, ameweka wazi kuwa mamlaka hiyo inaendelea na taratibu za ununuzi wa pampu mpya kwa ajili ya kufungwa kwenye mitambo ya uzalishaji wa maji. "Lengo ni kuboresha huduma na kuongeza kiwango cha uzalishaji ili kuhakikisha wakazi wengi wa Jiji la Dar es Salaam wanapata maji safi na salama kwa uhakika".
Kwa upande wake Meneja Uzalishaji Mtambo wa Maji Ruvu Juu Mhandisi Juma Kasekwa amesema marekebisho yaliofamywa ni katika pump na kuifanya mtambo wa Ruvu Juu kuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 196 kutoka lita milioni 122 kabla ya matengenezo
Naye Mkuu wa Kitengo Cha Mawasiliano DAWASA, Evarasting Lyaro amezungumzia kipande cha video ambayo imesambaa mtandaoni juu ya hali ya maji katika mto Ruvu ambapo amesema si ya kweli na imelenga kuleta taharuki kwani maji yapo ya kutosha na uzalishaji ni mkubwa.