Breaking

Monday, 24 March 2025

DKT.BITEKO AIPONGEZA EWURA USIMAMIZI WA AJIRA KWA WAZAWA



Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, ameipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa kusimamia vyema utekelezaji wa masuala ya ajira kwa wazawa (Local Content), hususan katika miradi mikubwa ya sekta ya nishati, ikiwemo Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Dkt. Biteko ametoa pongezi hizo leo, tarehe 24 Machi 2025, wakati akijibu hoja za wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini walioitaka Serikali kuhakikisha kuwa Watanzania wanapewa kipaumbele cha ajira katika miradi ya kimkakati ya sekta ya nishati

Dkt.Biteko ameeleza kuwa, EWURA imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha sera na miongozo ya ushiriki wa wazawa inatekelezwa kwa ufanisi, jambo ambalo limewezesha wazawa kunufaika na fursa za ajira na zabuni katika miradi mikubwa.

“EWURA imefanya kazi kubwa kuhakikisha watanzania wananufaika na fursa zilizopo katika miradi ya kimkakati kama EACOP. Naipongeza sana kwa kazi hii kubwa inayoendelea kufanya. Niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kusimamia sera za ushiriki wa wazawa ili kuhakikisha kuwa rasilimali za taifa zinawanufaisha wananchi wake,” alisema Dkt. Biteko.

Aidha, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya nishati ili kuimarisha ushiriki wa wazawa katika miradi yote inayoendelea na inayotarajiwa kuanza kutekelezwa nchini.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages