Breaking

Saturday, 8 February 2025

BALOZI NCHIMBI ASISITIZA UZINGATIAJI WA SERA NA MAADILI KWENYE CHAMA

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Mgombea Mwenza wa Urais Tanzania Bara, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amewahimiza wanachama wa Jumuiya ya Umoja wa Wazazi kuendelea kujipanga vyema ili kuhakikisha chama kinashinda kwa kuzingatia sera na maadili.

Akizungumza wakati akipokelewa kabla ya kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya hiyo jijini Dodoma, Dkt. Nchimbi alisisitiza kuwa CCM ni chama kinachojikita katika sera na maendeleo, si katika matusi au kejeli.

"Chama chetu kimefanya mambo makubwa kwa maendeleo ya taifa. Tunapaswa kuendelea kusimamia hoja zenye mashiko na si kutumia lugha zisizofaa. Tunapaswa kuwa mfano wa kuheshimu watu na kuzungumzia maendeleo yanayoonekana," alisema.

Aidha, alieleza kuwa serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanikisha mambo mengi ambayo yanaweza kuwahamasisha wananchi kuendelea kukiamini chama.

"Tunayo mengi ya kuwaambia Watanzania kuhusu maendeleo yaliyofikiwa, hatuna sababu ya kutumia lugha za kejeli. Hayo tuwaachie wale wasiokuwa na hoja za msingi," aliongeza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wazazi Taifa, Fadhili Maganya, alisema kuwa ujio wa Dkt. Nchimbi katika kikao hicho ni ishara ya heshima kwao.

"Uwepo wako hapa umetupa faraja kubwa. Tumekukaribisha ili usikilize mawazo yetu na kutushauri. Hii ni historia, kwani sisi ndiyo jumuiya ya kwanza kuketi na wewe tangu uteuliwe kuwa mgombea mwenza," alisema Maganya.

Kikao hicho kilitoa fursa kwa viongozi wa Umoja wa Wazazi kujadili masuala muhimu yanayohusu ustawi wa jumuiya na mchango wake katika mustakabali wa chama kuelekea uchaguzi ujao.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi akizungumza kwenye Kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la Umoja wa Wazazi, Jumuiya ya CCM, ambacho alialikwa na kushiriki akiwa mgeni maalum, leo Jumamosi tarehe 8 Februari 2025, katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages