Breaking

Sunday 20 October 2024

Ushirikiano wa UNESCO na Alwaleed Philanthropies Watangaza Mradi wa Maendeleo kupitia Utamaduni Nchini Tanzania

Na Rose Ngunangwa Dar Es Salaam

UNESCO kwa kushirikiana na Alwaleed Philanthropies, imezindua mradi unaolenga kuiwezesha jamii kutumia Utamaduni, Sanaa na Elimu ili kuleta Maendeleo endelevu nchini Tanzania.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa UNESCO nchiini Tanzania Bwana Michel Toto alibainisha hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati akifungua mkutano uliojumuisha wanufaika wa mradi huo.

Alisema, kupitia msaada wa kifedha na kiufundi kwa wanufaika hao, mradi huo unalenga kuleta matokeo endelevu kwa jamii watakayofanya nayo kazi

Kwa upande wake, Mratibu wa Utamaduni nchiini bwana Boniface Kadili alipongeza jitihada hizo na kusema kuwa utamaduni na elimu ya Sanaa vitasaidia kuhifadhi utajiri wa urithi wa utamaduni wa kipekee ulioko Tanzania na kurithisha vizazi vinavyokuja.

Mashirika yaliyochaguliwa kutekeleza mradi chini ya ufadhili huo ni TAMCODE, Mwanyanya Green Society, YAPO, SOMA na ADEA.

Mashirika haya yatatekeleza miradi yake Mkoani Katavi na Rukwa, Dodoma, Dar es Salaam, Mtwara na Zanzibar ambapo yamepita baada ya mchujo wa maandiko miradi takribani 38 yaliyowasilishwa UNESCO kwa ajili ya maombi ya ufadhili.

Alwaleed Philanthropies, inaongozwa na Binti wa Mfalme Lamia bint Majed Al Saud ambapo inafanya kazi duniani kote kupambana na umasikini, kujenga uwezo wa wanawake na vijana na kujenga maelewano kiutamaduni.

Mkutano huo ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka Wizara ya Habari, Vijana na Utamaduni kutoka Zanzibar, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bara, VETA, mashirika wanufaika, wafanyakazi wa UNESCO nchiini na Makao makuu Ufaransa pamoja na vijana wenye ushawishi mtandaoni.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages