Breaking

Tuesday 10 September 2024

SKANKA 1815 KG ZAKAMATWA KWENYE OPERESHENI ILIYOFANYWA NA DCEA DAR

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imekamata kilogramu 1,815 za dawa za kulevya aina ya skanka katika operesheni iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ukamataji huo uliohusisha watuhumiwa watano waliodaiwa kuhusika na dawa hizo umefanyika kupitia operesheni iliyofanyika Agosti 28 hadi Septemba 2 mwaka huu katika maeneo ya Luguruni Mbezi na Magomeni jijini Dar es Salaam

Akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 10,jijini Dar es Salaam Kamisha Jenerali wa DCEA Aretas Lyimo amesema watuhumiwa waliokamatwa ni pamoja na Richard Mwanri (47) ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Mbezi Makonde wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam na Felista Mwanri (70) mkulima na kazi wa Luguluni Mbezi wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam ambaye ni mmiliki wa nyumba zilipokutwa dawa hizo za kulevya.

Amesema watuhimiwa wengine ni Athumani Koja Mohamed (58) ambaye mfanyabiashara na mkazi wa Tanga, Omary Mohamed (32) dereva bajaji na mkazi wa Buza jijini Dar es Salaam na Juma Abdallah Chapa (36) mkazi wa Kiwalani jijini Dar es Salaam.

“Katika opereshen hiyo, gari aina ya Mitsubishi Pajero yenye namba za usajili T 551 CAB na bajaji yenye namba za usajili MC 844 CZV vilikamatwa,”amesema Kamishna Lyimo.

Kwa mujibu wa Kamishna Lyimo Richard Mwanri ni mhalifu ambaye amekuwa akipokea dawa za kulevya kutoka nchi mbalimbali na kuzingiza chini kwa usafiri wa magari zikiwa zimefichwa kwa kuchanganywa na bidhaa nyingine kisha kuzi sambazwa kwa wauzaji wengine katika maeneo mbalimbali chini.

“Kwa siku za hivi karibuni, dawa za kulevya aina ya skanka zimekuwa zikikamatwa mara kwa mara chini,skanka ni aina ya bangi ya iliyosindikwa yenye kiwango kikubwa cha kemikali yenye sumu aina ya Tetrahydrocannabinol (THC) ambayo inaweza kuharibu mfumo wa fahamu, akili na kusababisha magonjwa yasiyoambukiza kama vile moyo,figo na ini,”amesema Kamishna Lyimo.

Amesema matumizi ya skanka kwa wajawazito yanaweza kusababisha madhara kwa mtoto aliye tumboni ikiwemo kuathiri maendeleo ya ubongo na kuzaliwa na uzito mdogo.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages