Breaking

Sunday 22 September 2024

MNDEME AKAMILISHA UHAMASISHAJI WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KATIKA MIKOA MITANO


Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Christina Mndeme (katikati mbele) akiwasili mkoani Njombe kwa ajili ya kutoa elimu na uhamasishaji juu ya matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, Septemba 21,2024. Kushoto kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Njombe Mhe. Kissa Kasongwa na kulia kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Ludewa Mhe. Olivanus Thomas.

Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Christina Mndeme akivalishwa skafu na skauti mkoani Njombe mara baada ya kuwasili mkoani humo kwa ajili ya kutoa elimu na uhamasishaji juu ya matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, Septemba 21,2024.

Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Christina Mndeme akitoa elimu na uhamasishaji juu ya matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia mkoani Njombe Septemba 21,2024 ambapo mikoa mingine iliyonufaika na elimu hiyo ni pamoja na Katavi, Rukwa, Songwe na Mbeya.

Kamishina kutoka Wizara ya Nishati Bw. Styden Rwebangira akitoa elimu na uhamasishaji juu ya matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia mkoani Njombe, Septemba 21,2024.

Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Christina Mndeme amekamilisha ziara yake ya mkoa mitano ambayo alikuwa akitoa elimu pamoja na kuhamisha wananchi juu ya matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.

Akiwa mkoani Njombe Septemba 21, 2024 Bi. Mndeme amesema ziara hiyo imekuwa na mafanikio makubwa kutokana na mijadala, maswali na ushauri ambao wananchi walikuwa wakichangia kila siku baada ya uwasilishwaji wa maada mbalimbali.

Amesema baada ya kumaliza Katavi, Rukwa, Songwe, Mbeya na Njombe bado elimu itaendelea kutolewa sababu inahitajika zaidi ili kuhakikisha lengo la Serikali lililowekwa la kuhakikisha hadi mwaka 2034 asilimia 80 ya wananchi wawe wanatumia Nishati Safi ya Kupikia.

“Katika ziara hii tumegundua vitu vingi ikiwemo watu bado wanaamini Nishati Safi ni gharama kuitumia hasa taaasisi zile zinazolisha watu zaidi ya 100 wakihofia ufungaji wa mitambo.

“Hata hivyo hawaangalii athari zake ambazo zinatokana na matumizi ya nishati isiyokuwa salama, wengi wanaangalia unafuu wa upatikanaji wa nishati lakini hayo yote tumeyaona na yanafanyiwa kazi,” amesema Bi. Mndeme.

Kwa upande wake, Kamishina kutoka Wizara ya Nishati Bw. Styden Rwebangira ameeleza kuwa kila mmoja anapaswa kuliangalia jambo hili kwa kuijali afya yake na jamii inayomzunguka kwa kutumia Nishati Safi ya Kupikia.

Naye, Naibu katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu Bi. Felista Mdemu amesema jamii imeanza kuelewa taratibu umuhimu wa kutumia Nishati Safi ya kupikia japo elimu inapaswa kutolewa zaidi.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages