Breaking

Monday 26 August 2024

SERIKALI KUKUTANA NA WADAU KUJADILI HALI YA MAZINGIRA

Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais inatarajia kukutanisha wadau zaidi ya 1000 kwa ajili ya Mkutano wa kujadili na kuweka mikakati ya kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika tarehe 9-10 Septemba, 2024 Jijini Dodoma.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Agosti 26, 2024 Jijini Dar es Salaam, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Ashatu Kijaji amesema Mkutano huo Viongozi watakaoshiriki Mkutano huu ni Mawaziri na Makatibu Wakuu kutoka Wizara za Kisekta; Wakuu wa Mikoa; Wakuu wa Wilaya; na Wakurugenzi wa Halmashauri.

Aidha amewataja wadau wengine kuwa ni pamoja na Wizara na Taasisi za Serikali; Mashirika ya Umma, Sekta binafsi, vyuo vya elimu ya juu na Asasi zisizo za Serikali, Wakurugenzi kutoka katika mashirika ya Umma na wataalamu; Sekta Binafsi.

Dkt. Kijaji amesema Tanzania inakabiliwa na changamoto mbalimbali za mazingira ikiwemo uharibifu wa ardhi; uharibifu wa vyanzo ya maji; ukataji miti ovyo na uharibifu wa misitu; upotevu wa makazi ya wanyamapori na bayoanuai ambazo zimechangia kufifisha ustawi wa jamii na uchumi.

“Kwa kutambua mchango wa wadau katika kuhifadhi na kusimamia mazingira na mabadiliko ya tabianchi nchini, Ofisi ya Makamu wa Rais inaratibu Mkutano wa viongozi, wataalamu na wadau wa hifadhi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika tarehe 09 -10 Septemba, 2024 Jijini Dodoma” amesema Waziri Kijaji.

Ameongeza Mkutano huo unalenga kuimarisha uwajibikaji, ufanisi na usimamizi wa hifadhi ya mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na fursa zilizopo katika Biashara ya Kaboni; usimamizi wa taka; mabadiliko ya tabianchi; nishati safi ya kupikia; upandaji miti na usimamizi na uzingatiaji wa Sheria nchini.

Akifafanua zaidi Dkt. Kijaji amesema ni wajibu wa wadau mbalimbali kujitokeza katika kuunnga mkono juhudi za Serikali katika kuzuia uharibu wa mazingira ikiwemo utegemezi mkubwa wa kuni na mkaa kama chanzo cha nishati, kilimo kisicho endelevu, utupaji taka ovyo, na ufugaji wa mifugo usiowiana na maeneo ya malisho.

Kwa mujibu wa Dkt. Kijaji ameeleza kuwa Mkutano huo unatarajia kutoa taswira na mustakabali wa hali ya mazingira na ushiriki wa wadau na taasisi mbalimbali ikiwemo Serikali, sekta binafsi katika kukabiliana na hali ya uharibifu wa maizngira na mabadiliko ya tabianchi nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Ashatu Kijaji akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam kuhusu Mkutano wa kujadili tathimini ya hali ya mazingira nchini utakaofanyika Jijini Dodoma tarehe 9-10 Septemba, 2024.
Mkurugenzi Msaidizi wa Mazingira na Mabadiliko ya tabianchi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Deogratius Paul na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Bi. Sarah Kibonde wakifuatilia Mkutano wa Mhe. Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Dkt. Ashatu Kijaji (hayupo pichani) wakati akitoa taarifa kwa umma kuhusu Mkutano wa kujadili tathimini ya hali ya mazingira nchini utakaofanyika Jijini Dodoma tarehe 9-10 Septemba, 2024.

(NA MPIGAPICHA WETU)
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages