Breaking

Friday 23 August 2024

MHE. CHUMI AKUTANA NA KUZUNGUMZA NA NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA JAPAN

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Cosato Chumi (Mb) amekutana na kuzungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan Mhe. Kyoto Tsuji ofisini kwake jijini Tokyo.

Viongozi hao wamekubaliana kuendelea kushirikiana ili kuimarisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Japan kwa manufaa ya pande mbili.

Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Chumi aliishukuru Serikali ya Japan kwa kuendelea kuchangia maendeleo ya Tanzania katika sekta mbalimbali ikiwemo miundombinu, uwekezaji, elimu, na afya.

Amesema Tanzania imejipanga kuhakikisha inaongeza kiwango cha biashara na uwekezaji kati yake na Japan na hivyo kuchochea ukuaji wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa manufaa ya pande zote mbili.

Naye, Mhe. Tsuji ameelezea utayari wa Japan kuendelea kushirikiana na Tanzania na kuimarisha uhusiano uliopo kwa manufaa ya nchi hizo.

Amesema Japan itaendelea kushirikiana na Tanzania na kuongeza biashara na bara la Afrika ili kuhakikisha maendeleo ya kweli yanapatikana.

Mhe. Chumia yuko nchini Japan kuhudhuria Mkutano wa Tisa wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD) ngazi ya Mawaziri utakaofanyika jijini Tokyo tarehe 24-25 Agosti 2024.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages