Breaking

Monday 1 July 2024

RC KIHONGOSI APIGA MARUFUKU UTUMIKISHWAJI WANAFUNZI MASHAMBA YA WALIMU



Kisesa-Meatu.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Kenan Laban Kihongosi amepiga marufuku utumikishwaji wa Wanafunzi katika mashamba binafsi ya Walimu Mkoani Simiyu

Mhe.Kihongosi ametoa marufuku hiyo aliposikiliza kero za Wananchi katika Kijiji cha Mwaukoli Kata ya Kisesa Wilayani Meatu.

Wananchi wa Mwaukoli wamemueleza Mkuu wa Mkoa Kihongosi kuwa kumekuwepo changamoto ya utumikishwaji wa Wanafunzi katika mashamba binafsi ya Walimu katika eneo hilo wakitolea mfano Shule ya Msingi Mwaukoli.

Alipotakiwa kutoa maelezo juu ya tuhuma zilizotolewa na Wananchi juu ya utumikishwaji wa Wanafunzi katika Shule ya Mwaukoli,Afisa wa Elimu Kata ya Kisesa Bw.Jibende Kanga alikataa kuwepo kwa Tabia hiyo na kwamba hakuwahi kupokea malalamiko yoyote kuhusu tuhuma hizo.

Hata hivyo mchungaji Lucas Ruvanga wa Kanisa la Adventista wa Sabato Kijiji Mwaukoli alitoa ushuhuda wa namna ambavyo Watoto katika eneo hilo wamekuwa wakitumikishwa.

Kufuatia ushuhuda huo Mkuu wa Mkoa Kihongosi akaelekeza uongozi wa Halmashauri Wilayani Meatu kuhakikisha Wanasimamia na kufuatilia kwa karibu ambapo amesema hatosita kuchukua hatua kwa Mwalimu yeyote atakayebainika kutumikisha watoto katika Mashamba.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Kenan Kihongosi yuko katika ziara Wilayani Meatu kwa ajili ya ukaguzi wa Miradi na kusikiliza kero mbalimbali za Wananchi.

SIMIYU-RS

01 Julai 2024.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages