Breaking

Wednesday 3 January 2024

DAWASA KIBAMBA YAJIPANGA KUFIKIA WENGI ZAIDI 2024





Mamlaka ya Majisafi ya Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) kupitia mkoa wa kihuduma Kibamba umejipanga kuwafikia wateja takribani 20,000 kwa mwaka 2024 kutoka wateja 15,000 wanaowahudumia sasa kwa lengo la kutimiza adhma ya Mamlaka ya kuwafikia wote ifikapo 2025.

Matarajio hayo yamesemwa na Afisa Biashara wa mkoa wa DAWASA Kibamba, Ndugu Ian Mlay ambapo amesema mikakati iliyopo ili kuwafikia wateja 5,000 zaidi ikiwa ni pamoja na kufanya miradi midogomidogo ya kuwaunganishia wateja huduma baada ya kukamilisha miradi mkubwa mojawapo ukiwepo Mradi wa maji Mshikamano.

"Moja ya mipango wetu ni kuhakikisha tunawafikia wateja wote wa eneo tunalolihudumia kwa kuongeza wigo wa mtandao wetu wa huduma, tunawaomba wateja wetu wasisite kuleta maombi ya kuunganishwa na huduma zetu" amesema Ndugu Mlay

Pia amesema malengo mengine ni pamoja kupunguza idadi ya wateja wenye madeni ya muda mrefu kwa kuingia makubaliano maalum ili waweze kulipa huduma kidogo kidogo huku wakiendelea kupata huduma ya maji.

"Tunaendelea kuwasihi wateja wetu kulipia huduma kwa wakati na kutokusubiri kusitishiwa huduma ambapo ulipaji wa bili zetu kunachangia maendeleo kwa maeneo mengine ambayo bado hayajapata huduma." amesisitiza Ndugu Mlay

Aidha DAWASA Kibamba imejikita katika kuendeleza mashirikiano baina yake na wateja kwa kutoa elimu na taarifa mbalimbali kupitia makundi sogozi ikiwemo mitandao wa Whatsapp, Mitandao rasmi ya kijamii ya DAWASA na Kituo cha Huduma kwa wateja.

Mkoa wa kihuduma Kibamba unahudumia Kata 5 ambazo ni Msigani, Kwembe, Kiluvya, Kibamba na Sehemu ya kata ya Mbezi. Ofisi za DAWASA Kibamba zinapatikana eneo la Mbezi Luguruni karibu na ofisi ya Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo.





Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages