Na Mwandishi, Rukwa
MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imeeleza kwamba imekuwa ikiendesha vikao na wadau bandari wakiwemo wafanyabiashara ili kukaa kwa pamoja na kuangalia namna ya kutatua changamoto za kiutendaji na hatimaye huduma kuendelea kuboreshwa zaidi.
Kauli hiyo imetolewa Juni 4 mwaka huu na Meneja wa Bandari za Ziwa Tanganyika, Edward Mabula alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea bandari hiyo kwa lengo la kuona shughuli mbalimbali pamoja na maboresho yaliyofanywa na Serikali kupitia TPA za kuboresha miundombinu.
Amesema jitihada za kufanya vikao na wadau pia zimefanyika pia katika bandari ya Kabwe wilayani Nkasi mkoani Rukwa na sababu za kufanya vikao hivyo ni kuendelea kuvutia zaidi wateja kutumia bandari hiyo inayohudumia zaidi nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi kwa kusafirisha bidhaa za vyakula na vifaa vya ujenzi hususani saruji.
Amesema bandari hiyo inayohudumia hadi tani 1,200 za mizigo pamoja na abiria 400 kwa mwezi pamoja na mafaniko bado kuna baadhi ya changamoto ambazo zinazokikabili bandari hiyo ikiwemo miundombinu ya barabara kutokuwa mizuri
Amefafanua changamoto katika bandari ya Kabwe ni miundombinu ya barabara ya kuja bandarini haiko vizuri sana, hivyo wangetamani kuona inawekwa lami ili kuvutia wateja zaidi.
“Bandari ya Kabwe ni kiungo muhimu kwa shughuli za biashara na kiuchumi kwa nchi za Tanzania, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi,”amesema Mabula .
Kwa upande wake Manda Silvester ambaye ni Wakala wa Forodha katika bandari hiyo ametumia nafasi hiyo kuelezea kufurahishwa kwake na huduma za bandari hiyo huku akiipongeza TPA na Serikali kwa ujumla kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya bandari.
“Kwa sasa upakiaji na upakuaji mizigo katika bandari hii muda wake umepungua hadi kufikia siku moja huku vyombo vya usafiri kufika moja kwa moja kwenye jeti na tofauti na awali mizigo ilikuwa inapakiwa na kupakuliwa mbali na bandari.”
Wakati huo huo Edward ambaye pia ni Wakala wa Forodha ameiomba serikali kupitia TPA kuliangalia suala la barabara inayoingia bandarini kwani ni changamoto kwa wateja wanaotaka kwenda bandarini, hivyo ni vema Serikali ikaangalia namna ya kuiboresha ikiwezekana kuwekewa lami ipitike kwa urahisi zaidi.
Bandari ya Kabwe ni miongoni mwa bandari tatu katika Mkoa wa Rukwa ambayo inapatikana wilani Nkasi ambayo ujenzi wake umegharimu Sh.bilioni 7.4.







