Breaking

Wednesday 12 October 2022

AJERUHIWA VIBAYA BAADA YA KUKATA NGUZO YA UMEME KWA SHOKA



Na Lucas Raphael,Tabora

Kijana mmoja aliyetambulika kwa jina la Kigodi Juma (24)amejeruhiwa vibaya maeneo ya mwili wake baada ya kupingwa na shoti ya umeme alipokuwa akifanya hujuma ya kukata nguzo ya umeme kwa kutumia shoka.

Mtu huyo ambaye ni mkazi wa kijiji cha Nkiniziwa kilichopo Wilaya ya Nzega Mkoani Tabora .

Akitoa ufafanuzi wa tukio hilo Afisa mtendaji wa kata ya Nkiniziwa Hamisi Bundu alisema kijana huyo alitenda tukio hilo usiku wa kuamkia Oktoba 11,2022 ambapo kunako majira hayo ya usiku walishitushwa na kukatika kwa huduma ya umeme.

Alisema kijana huyo kabla ya kuanza kukata nguzo hiyo alirusha waya uliokuwa umefungwa vipande vya miti kwa ajili ya kupigisha shoti ili umeme uweze kukatika ili apate urahisi wa kuangusha nguzo hiyo bila wasiwasi wa kujeruhiwa na umeme pasipo kujua kama umeme bado ulikuwa haujakatika.


Hamisi Bundu aliendela kusema kwamba baada ya kijana huyo kukata nguzo hiyo na kisha kupigwa shoti na moto kali wa umeme kutokea kwenye la eneo la tukio hilo.

Alisema kwamba kijana huyo ambaye alishambuliwa vibaya na shoti ya umeme alikimbizwa katika kituo cha afya Busondo ambacho kipo jirani na kijiji hicho ambapo kwa sasa anaendelea na matibabu.

Naye kaimu Mganga wa kituo cha afya Busondo Juma Sosoma alikiri kumpokea majeruhi huyo ambaye aliangusha nguzo ya umeme.

Alisema kwamba licha ahuweni aliyonayo kwa sasa ataandikiwa rufaa ya kwenda katika hospitali kubwa kwa ajili ya vipimo zaidi vya ndani ya mwili kutokana na kuumia vibaya katika maeneo ya miguu,shingo ,usoni na kwenye mikono.

Wanachi wa kijiji cha Nkiniziwa walisema mpaka sasa bado wanaendelea kuathirika na ukosefu wa huduma ya umeme huku tukio hilo la kukatwa kwa nguzo likitajwa kuwa ni la pili katika eneo hilo hilo.

Kaimu meneja wa shirika la umeme nchini TANESCO katika Mkoa wa Tabora Mhandisi Hamisi Maganga alisema shirika linaendelea na ufatiliaji wa kina juu tukio hilo huku akiwaonya vikali wananchi dhidi vitendo vya kufanya kuhujumu miundombinu ya umeme .

Kamanda wa Polisi ACP Richard Abwao alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kwamba mtuhumiwa anaendelea na matibabu licha ya kuumia vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake .

Alisema kwamba jeshi la polisi linaendelea na upelelezi wa kuwatafuta watuhumiwa wengine walioshiriki katika kuharibu miundombinu ya umeme na kuongeza hii ni mara ya pili kwa nguzo ya umeme kukatwa kwenye eneo hilo .



mwisho

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages