Breaking

Thursday 28 July 2022

TUME YA MADINI YAZIDI KUSHIKA KASI, YAKUSANYA BILIONI 623




Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai 2021 hadi Juni, 2022 tume imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 623 ikiwa ni sawa na asilimia 95.88 ya lengo la kipindi husika ambapo ilipangiwa kukusanya shilingi bilioni 650.

Mhandisi Samamba aliyasema hayo katika kikao cha 15 cha Tume ya Madini kwenye taarifa ya mwaka wa fedha 2021/2022 ya utendaji wa Tume ya Madini aliyoiwasilisha leo katika kikao cha Tume chenye lengo la kupokea na kujadili taarifa ya utendaji kwa kipindi husika.

Alisema kuwa siri ya mafanikio hayo ni pamoja na utendaji kazi wa pamoja, kupanua huduma za Tume ya Madini kupitia uanzishwaji wa Ofisi mpya za Kimadini za Mikoa katika maeneo ya Mbogwe Mkoani Geita, na Songwe; masoko ya madini kuongezeka hadi kufikia 42 na vituo vya ununuzi wa madini 77 vilivyoanzishwa.

Akielezea mikakati ya Tume ya Madini katika kuhakikisha inavuka lengo la ukusanyaji wa maduhuli la shilingi bilioni 822 lililowekwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2022/2023, alisema kuwa Tume ya Madini imebuni vyanzo vingine vya mapato ikiwa ni pamoja na migodi ya uchimbaji mkubwa, wa kati na mdogo inayotarajiwa kuanzishwa pamoja na kuimarisha usimamizi kwenye ukusanyaji wa mapato yanayotokana na madini ujenzi na viwandani.

Wakati huohuo akielezea kasi ya utoaji wa leseni za madini katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022, Kamishna wa Tume ya Madini, Profesa Abdulkarim Mruma alisema kuwa Tume imevuka lengo kwa kutoa leseni za madini 9498 sawa na asilimia 109.5 ya lengo la kipindi husika.

Naye Kamishna wa Tume ya Madini, Janet Reuben Lekashingo akielezea mafanikio kwenye Ushirikishwaji wa watanzania katika Sekta ya Madini alisema katika kipindi cha mwezi Aprili hadi Juni 2022, jumla ya mipango 154 ya Ushirikishwaji wa Watanzania kwenye Sekta ya Madini iliwasilishwa na mipango 153 imeidhinishwa baada ya kukidhi vigezo.

Alifafanua kuwa ongezeko la maombi yanayopitishwa limetokana na elimu ambayo imekuwa ikitolewa na Tume ya Madini kwa wadau hususan wamiliki wa migodi na watoa huduma kwenye migodi.

“Tume ya Madini kupitia kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania kwenye Sekta ya Madini itaendelea kutoa elimu ili kuhakikisha matakwa ya kisheria ya Ushirikishwaji wa Watanzania kwenye Sekta ya Madini yanazingatiwa,”alisema Lekashingo.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha kikao hicho, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula alipongeza kasi ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, menejimenti na watumishi wote kwa utendaji mzuri unaoendelea kujenga taswira chanya ya Tume ya Madini.

"Kiukweli napongeza kasi nzuri mno ya utendaji wa Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, menejimenti, watumishi wote kwa ujumla, mnanifurahisha mnoo, endeleeni kuchapa kazi, tutaendelea kufanyia kazi changamoto zilizopo na zitakazojitokeza" alihitimisha Profesa Kikula.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages